Simulizi : muuaji asakwe...... sehemu ya Tatu

 Mtunzi ni: Patrick J. Massawe


Utangulizi


Mwanamke mrembo anauawa ndani ya bafu, nyumbani kwake, eneo la Tabata, Jijini Dar es Salaam. Kwanza kabisa, muuaji huyo katili alimtumia ujumbe wa vitisho muda mfupi tu kabla ya kutekeleza mauaji hayo. Pia, muuaji huyo alimbaka mrembo huyo kabla ya kumuua. Upelelezi wa Jeshi la Polisi, unafanyika mara moja. Msako mkali dhidi ya muuaji huyo unafanyika, na inagundulika siri nzito iliyojificha nyuma ya mapazia kuhusiana na kifo hicho chenye utata. Kama kawaida, mtunzi wako mahiri,  PATRICK J. MASSAWE anatiririka na hadithi hii ya kusisimua.     Fuatilia mpaka mwisho wake…



Getruda kwenye sofa lililokuwa pembeni.


“Haya…nakaa..” Getruda akamwambia huku akikaa.


“Hayo si ndiyo maneno?” John Bosho akamwambia huku naye akikaa kando yake. Chumbani hapo palikuwa kimya, isipokuwa ni sauti ndogo ya runinga ndiyo ilikuwa inasikika.


Baada ya kukaa kwa muda, John Bosho aliagiza vinywaji na mapochopocho kwa mhudumu maalum aliyekuwa anamhudumia kila mara anapokuwa anafika hapo. Wakaendelea kula na kunywa na huku wakiongea mambo mengi tu, kitu ambacho kilimshangaza Getruda, kwani John hakumwambia alichokuwa anamwitia!


“Shemeji John…” Getruda akamwita John kwa sauti ndogo.


“Naam shem…” John Bosho akaitikia huku akimwangalia Getruda.


“Naona muda unazidi kwenda…”


“Ni kweli unakwenda…”


 “Basi, naomba unieleze ulichoniitia…”


“Hakuna taabu. Nitakueleza tu…” John  Bosho akamwambia huku akiwaza la kufanya.


Ni kweli kwamba John alikuwa amemwita pale kwa ajili ya mazungumzo maalum na yeye, lakini tokea amefika, ameshindwa kumwambia alichomwitia zaidi ya kuonyesha matamanio tu kuuangalia mwili wake! Kwa vile alikuwa amedhamiria kumpata kimapenzi, shemeji yake huyo, Getruda, aliamua kufanya kitu kimoja kibaya sana.


Alipanga kuwa kabla ya kumwelezea kile alichomwitia, ni lazima afanye jambo fulani, ambalo litamlainisha mwanamke huyo aliyempania kupita kiasi. Yeye alikuwa ameshajiandaa kwa chochote tokea alipofika katika eneo lile husika. Hivyo aliamua kumtilia Getruda dawa ya usingizi, kwenye kinywaji chake, ambayo ni dawa yenye uwezo wa kumlegeza mwili wake haraka.


“Hebu naomba unieleze shemeji, maana unaniweka roho juu kwa kusubiri…” Getruda akaendelea kumwambia John Bosho


“hakuna taabu, shem, nitakueleza, kwani si jambo bay asana, mpaka likuweke roho juu sana…” John Bosho akamwambia.


“Sawa, ngoja nikajisaidie, nikirudi basi unieleze ili roho yangu itulie…” Getruda akamwambia huku akinyanyuka kuelekea msalani.


“Na kweli, utasuuzika na roho yako…”


Hivyo basi, mara baada ya Getruda kwenda kujisaidia ndani ya choo kilichokuwa mlemle chumbani, John Bosho alibaki akishangilia sana, huku akirusha ngumi yake hewani, akijua kuwa sasa mpango wake utafanikiwa, ni lazima atafune kitu roho inapenda!


Hakupoteza muda, kwani John alichukua ile dawa ya usingizi, iliyokuwa katika asili ya unga mweupe hivi. Akaunyunyuzia ndani ya glasi iliyokuwa na kinywaji alichokuwa anakunywa Getruda, halafu akamsubiri mpaka atakaporudi kutoka msalani!


      ********


HAIKUCHUKUA muda mrefu, Getruda alirudi kutoka msalani. Akafikia tena kwenye sofa na kuiangalia glasi yake iliyokuwa na pombe nusu, lakini hakuinywa kwanza, bali alimwangalia John Bosho aliyekuwa anamwangalia kwa uchu mkubwa.


Hata hivyo Getruda hakuweza kugundua mpango ule aliokuwa ameupanga John Bosho. Hivyo akainyanyua ile glasi na kunywa kinywaji kile cha bia kilichokuwa na mchanganyiko wa dawa ya usingizi aliyokuwa amemwekea, na alipomaliza kunywa, akaitua glasi chini.


“Shemeji…” Getruda akamwita.


“Naam…” John akaitikia.


“Nafikiri mimi nikimaliza kinywaji hiki, naondoka…”


“Unaondoka kabla sijakueleza nilichokuitia?”


“Usiondoke,” John Bosho akamwambia na kuongeza. “Basi, nitakueleza, tega sikio!”


Hata hivyo, kabla John hajaanza kumwelezea alichomuitia pale, dawa ile ikaanza kumlegeza na kumfanya kama amelewa kiasi cha kushindwa kustahimili, naye  John alipoona Getruda amelegea, ndipo alipoanza kumweleza alichomuitia.


“Shemeji Getruda…” John akamwita.


“Eeee…shem…” Getruda akaitikia kwa sauti ya kilevi.


“Unajua nilichokuitia?”


“Hapana…sijui…”


“Nisikilize…”


“Nakusikiliza…oh!”


“Unajua nakupenda?”


“Oh….unanipenda?”


“Ndiyo. Nakupenda shem…”


“Unanipenda kivipi?”


“Nakuhitaji. Nataka uwe mpenzi wangu…”


“Shemeji…ah! Haiwezekani…na Anita je?”


“Mambo ya Anita achana naye kwa wakati huu!”


“Nisijali vipi wakati ni mchumba wako?” Getruda akasema na kuongeza. “Isitoshe ni rafiki yangu!”


“Nimeshakwambia hayo usijali…”


“Ah, shem unaniweka katika wakati mgumu…”


John Bosho akiwa na ulimi wa kushawishi, kubembeleza na pia ukichangia na ile dawa aliyomwekea Getruda ndani ya kinywaji chake, akaendelea kumbembeleza. Akahamia katika sofa alilokalia Getruda, akifanikiwa kumshawishi na kukubaliana kukutana kimapenzi! Dakika tano zilizofuata, wote walikuwa wameshasaula nguo zao na kubaki kama walivyozaliwa!


Wakajikuta pia wakigaragara katika kile kitanda kikubwa cha futi sita kwa sita ikifuatiwa na miguno hafifu ya kimahaba mazito! Baada ya kumaliza ile mechi nzito, kila mmoja alijitupa kivyake na hatimaye Getruda kupitiwa na usingizi mzito kutokana na ile dawa aliyokuwa ametiliwa kwenye kinywaji.


John Bosho aliufurahia ule ushindi wa kumpata kiumbe yule husika aliyekuwa na matamanio naye kwa muda mrefu, akajipongeza kwa hilo huku akiendelea kumwangalia zaidi na zaidi pale juu ya kitanda alipokuwa amejilaza Getruda katika umbile lile la utupu alilokuwa nalo! Ni hatari sana!


Getruda alijikuta akilala ndani ya chumba kile alichopanga John Bosho. Ni mpaka ilipotimu saa nne za usiku ndipo aliposhtuka kutoka kwenye usingizi mzito na kujikuta amelala kwenye kitanda kimoja na John, shemeji yake! Ni usaliti wa hali ya juu!


“Oh! Shem John!” Getruda akaita huku akinyanyuka kutoka pale kitandani nusu akipepesuka!


“Naam,” John Bosho akaitikia huku akimwangalia kwa kijicho pembe!


“Aisee? Umefanya nini?” Getruda akamuuliza huku akijiangalia katika hali ile ya utupu aliyokuwa nayo!


“Kwani vipi?”


“Huoni kama tumemsaliti Anita?”


“Kumsaliti?”


“Ndiyo manaake!”


“Hayo usijali sana…” John Bosho akasema huku akitabasamu na kuonyesha ujivumi kwa kumpata na kujifurahisha kingono!


“Nimefanya kosa kubwa sana…haya… nirudishe nyumbani!” Getruda akasema huku amechukia!


“Nenda kaoge mpenzi…” John Bosho akamwambia.


“Mpenzi tena…ala!” Getruda akamwambia huku akijifunga taulo kubwa.


“Kwani kosa kukuita mpenzi?”


“Ah, tuyaache hayo!”


Getruda akaingia bafuni ambapo alioga haraka haraka na kutoka. Halafu John naye akaingia na kuoga, huku akimwacha Getruda akijiandaa kuvaa nguo zake. Baada ya kumaliza kuvalia, wakatoka hadi nje ambapo walipanda gari la John, tayari kwa kumrudisha Getruda nyumbani kwake, mtaa wa Moshi, Ilala.


Walipofika nyumbani kwa Getruda, ilikuwa imetimu saa saa tano za usiku, na pilikapilika za watu zilikuwa bado zinaendelea katika mitaa ile ya Ilala, na nyumba aliyokuwa anaishi Getruda, ilikuwa bado haijafungwa.


Kabla ya kushuka garini, John Bosho akamkabidhi Getruda kitita cha fedha,  shilingi laki tatu, ambazo zilitosha kumlegeza. Akasahau mambo yote yaliyotokea nyuma, na wala hakugundua kama John alikuwa amemtilia dawa ya kulevya katika kinywaji chake ili aweze kutimiza azma yake ya kufanya naye mapenzi!


Basi, tokea siku ile ndiyo ukawa mchezo wao, ambao uliwafanya wanogewe na kuwa wanakutana mara kwa mara kwenye nyumba mbalimbali za wageni na kuivunja amri ya sita. Hata hivyo iliwabidi wafanye mambo yao kwa siri sana, ili Anita asiweze kuwashtukia, wakijitahidi kusafiri sehemu za mbali na kukamilisha kiu yao.


Kutokana na ubize aliokuwa nao Anita, hakuweza kuwashtukia kabisa, kama rafiki yake mkubwa, Getruda, alikuwa amemchukulia mchumba wake, John Bosho. Kila mmoja aliendelea na shughuli zake na siku zikawa zinasonga mbele. Lakini hakuna marefu yasiyokuwa na mwisho!


        ********


JUMATATU moja ambayo ni mwanzo wa wiki, Anita alikuwa amekaa ndani ya ofisi yao, pamoja na mfanyakazi mwenzake, Magret. Alionekana ni mtu mwenye mawazo mengi sana tangia alipoingia kazini asubuhi, kiasi cha kushindwa hata kufanya kazi. Pia, alikuwa ni mtu wa kujifyonza mwenyewe, ikionyesha kuwa kuna kitu alikuwa anawaza!


Ndipo Magret alipoamua kumsogelea karibu ili amuulize kulikoni mpaka awe katika hali kama ile ambayo siyo kawaida yake. Anita siku zote alikuwa ni mtu mcheshi na mchangamfu kwa kipindi chote cha kazi, na kila mmoja alimzoea hivyo.


“Vipi Anita, unaumwa?” Mage alimuuliza.


“Hapana, mimi siumwi…” Anita alimwambia Magret huku akimwangalia kwa sura ya huzuni.


“Sasa mbona uko katika hali kama hii?” Magret akaendelea kumuuliza.


“Ah, wewe acha tu Mage…” Anita akasema kwa sauti ndogo ya huzuni.


“Niache nini wakati nakuona hauko sawa?”


“Ni kweli Mage…siko sawa…”


“Ni kitu gani kinakusumbua?”


“Kuna kitu kinanisumbua,” Anita akamwambia na kuongeza. “Lakini hakifai kuongelea hapa ofisini Magret.”


“Kwa hivyo tukaongelee wapi?”


“Naona twende hapo The Kibo II Hotel, ambayo ni sehemu nzuri…” Anita alimwambia huku akinyanyuka kutoka kwenye kiti.


“Haya, twende…” Magret akamwambia Anita.


Anita na Magret walitoka pale ofisini na kuelekea The Kibo II Anex Hotel, ambayo haikuwa mbali na pale. Baada ya kuingia ndani, wakaagiza vinywaji baridi na kuendelea kunywa taratibu.


“Ndiyo ndugu yangu, naona kuwa huu ni muda muafaka wa kunielezea kilichokusibu…” Magret akamwambia Anita.


“Ni sawa, inabidi nikuelezee kila kitu, kwa vile wewe ni mtu wangu wa karibu…” Anita akamwambia Mage huku uso wake ukionyesha bado kuwa na huzuni.


“Nieleze mwaya, huwenda nikapata wazo la kukusaidia…”


“Hivi si unajua kuwa nina mchumba?”


“Ndiyo, najua kuwa unaye mchumba.”


“Lakini tatizo ni kwamba mchumba wangu huyo ananipa taabu sana.”


“Shida gani tena?”


“Ananitesa sana, sijui kwa vile anajua kuwa ninampenda? Maana nasikia anajihusuisha kimapenzi na shoga yangu, Getruda…”


“Unasema kweli?”


“Ninasema kweli, kwa sababu siku hizi ninaona wana ukaribu mkubwa sana.”


“Hali hiyo imeanza lini?”


“Imeanza mara baada ya mimi kumtambulisha kwake.”


“Je, una uhakika wana mahusiano?”


“Dalili zinaonyesha na pia nimeshauona ujumbe wa simu kwenye simu ya John Bosho. Hata hivyo alijitahidi kuukwepesha.”


“Ulishawahi kumuulizia Getruda juu ya tuhuma hizo?”


“Hapana, sijamuuliza…”


“Vizuri sana. Usimuulize kwanza, jaribu kufanya upelelezi kwanza na utakapogundua, ndipo utakapomweka kitako na kumuuliza.”


“Sawa Mage, nitajitahidi kufanya upelelezi juu ya hayo. lakini roho inaniuma sana… si unajua kuchukuliwa mwanaume kunavyouma?”


“Ni kweli kunauma sana, lakini ushauri ndiyo huo, fanya upelelezi kwanza! Mambo mengine yatafuata.”


“Sawa, nitafanya hivyo.”


Baada ya kumaliza mazungumzo yao, Anita na Magret walitoka pale hotelini na kurudi ofisini kwao. Kwa kiasi fulani Anita alikuwa ameridhika na tabasamu pana lilionekana usoni mwake.


********


HAKUNA siri ya watu wawili duniani. Anita alikuja kuujua ule uhusiano wa kimapenzi baina ya Getruda na mchumba wake, John Bosho. Aligundua hilo baada ya kudokezewa na kijana mmoja, mwendesha bodaboda, aliyeujua uhusiano ule usiokuwa rasmi. Yeye alikuwa akimbeba mara kwa mara  Anita, kumpeleka katika sehemu mbalimbali ambazo alihitaji kufika haraka.


Basi, akiwa katika kazi zake za kubeba abiria, ndipo kijana huyo alipoweza kuuona ule uhusiano wa Getruda na John Bosho, walivyokuwa wakijirusha na kutanua. Roho ikamuuma sana  kwa vile alikuwa anamheshimu Anita kama dada yake wa kuzaliwa tumbo moja. Hakuvumilia, hivyo akaamua kummwagia siri ile!


Kijana huyo mwendesha bodaboda maarufu, alijulikana kwa jina moja tu, Don, ambalo ni jina alilokuwa amekatiwa na vijana wenzake wa mtaani, na wala jina la pili halikujulina. Yeye alikuwa akifanya kazi ile kati ya maeneo ya Buguruni Shell na maeneo ya Tabata, na mara nyingine sehemu mbalimbali za jiji, kama atakuwa amepata mteja wa kumpeleka huko. 


Baada ya Don kumfikishia ujumbe huo Anita, alimshukuru sana kwa kumtoa tongotongo machoni mwake, kwani alikuwa hajui kitu kama hicho. Hivyo akaamua kuufanyia kazi, na pia kupanga kumpa kazi nyingine ya kuendelea kumpeleleza John Bosho bila yeye kufahamu. Vilevile hakuacha kumjulisha rafiki yake, Magret juu ya kuinyaka siri hiyo, ambaye naye alimpatia ushauri wake, kuwa ni vyema angeanza kufanya upelelezi wake binafisi, na hata kumtumia Don.


Na kweli, Anita aliamua kuanza kufanya upelelezi huo mara moja, baada ya kupewa ushauri na huyo Mage, mfanyakazi mwenzake. Pia, kwa bahati nzuri  Don, naye alikuwa anaujua uhusiano wa Anita na John, kama ni mtu na mchumba wake na mara nyingine aliwaona wakiambatana wote katika kilele cha mapenzi yao.


Hivyo basi, siku moja Anita alimkalisha kitako Don na kuanza kuongea naye kumwelezea masahibu yaliyompata, ambapo alitaka msaada wake wa hali na mali katika kukamilisha upelelezi wake.


“Kaka yangu, Don…” Anita alianza kumwambia.


“Naam, dada yangu,” Don aliitikia huku akimwangalia kwa makini.


“Samahani sana, leo nina mazungumzo muhimu sana na wewe,” Anita akaendelea kumwambia Don.


“Mazungumzo gani dadangu?”


“Ni mazungumzo yanayonihusu mimi na mchumba wangu, John Bosho. Natumaini unatambua kuwa uhusiano wangu naye.”


“Ndiyo, uhusiano wako na John mimi naufahamu…”


“Hivyo basi, nakuomba nikushirikishe huenda ukanipa ushauri cha kufanya…”


“Unaweza kunieleza dada, kama kuna ushauri bila shaka nitakueleza cha kufanya.”


“Natumaini unamfahamu vizuri mchumba wangu, John Bosho…”


“Ndiyo, namfahamu. Si yule anayeendesha gari aina ya Toyota Harrier?”


“Ndiye huyo huyo!” Anita akamwambia na kuendelea. “Ni mchumba wangu, ambaye tumevishana pete za uchumba. Lakini mwenzangu kwa kiasi fulani amekuwa siyo mwaminifu, nasikia anatembea na rafiki yangu, Getruda, anayeishi kule, Ilala!”


“Unasema kweli dada?” Don akamuuliza huku ameachama mdomo!


“Ni kweli kabisa. Hivyo basi, nakuomba uwe unafuatilia nyendo zao kwa vile wewe ni dereva wa pikipiki, hawataweza kukushtukia kamwe. Na hiyo ni ili tujue kama kinachozungumzwa ni kweli wana mahusiano, najua kwa vile unayo hiyo pikipiki, kazi haitakuwa ngumu sana. Hilo ndiyo ombi langu, siyo kama ninakulazimisha,” Anita akamaliza kusema huku akimwangalia kwa uchungu mwingi Don.


“Nimekuelewa dada Anita, kwa hicho ulichonieleza. Kumbuka kuwa mimi ni mwanaume, na sipaswi kuwa mmbea, lakini kwa shida uliyoipata, sina budi kukusaidia…” Don alimwambia Anita.


“Nitashukuru sana,” Anita akasema huku akitabasamu tabasamu la uchungu.


“Tena,” Don akaendelea kusema. “Mimi nimeshawahi kuwaona wakiwa katika sehemu mbalimbali za stareha, lakini sikujua kama walikuwa na mahusiano ya kimapenzi kabisa. Lakini maadam aumeniambia hivyo, sina budi kukusaidia…” Don akaendelea kumwambia Anita.


“Nitashukuru sana kakangu. Fuatilia na kila utakachokiona, nifahamishe, nitakutoa kwa chochote…” Anita akamwambia Don.


“Ah, hayo usijali dada, wewe wangu,” Don akamwambia.


Baada ya maongezi yao, Anita na Don waliagana kila mmoja akaendelea na shughuli zake.


Siku hiyo ikapita!


Mara baada ya Anita kuzipata taarifa za mchumba wake, John Bosho, alichanganyikiwa sana. Ili kuuokoa ule uhusiano wao wa uchumba, alimkabili na kumuulizia kuhusu tetesi zile, lakini John aliruka na kusema kwamba yale yalikuwa ni maneno ya watu tu yasiyowatakia maendeleo yao. Kamwe John  hakukubali kabisa kujihusisha kimapenzi kwa rafiki yake, Getruda.


Anita alinyamaza kimya huku akiendelea kufanya uchunguzi wake. Daima alijua kuwa njia ya mwongo ni fupi, na iko siku lazima atakuja kuwafumania wakiwa wawili, ndiyo, ni lazima!


Aliapa!


********


MIEZI mitatu ilipita tokea John Bosho na Anita walipoanza kuulizana juu ya ule usaliti wa mapenzi uliokuwa ukifanyika. Hata hivyo kila mmoja aliendelea na kazi, ambapo Anita alikuwa alijaribu kwa hali na mali kuyasahau yale yaliyopita nyuma, hasa ukizingatia kazi aliyokuwa anafanya, ilikuwa ikimweka bize sana.


Kila alipokuwa anatoka kazini huwa anachoka sana kiasi kwamba akifika nyumbani ni kupika, kuoga na kulala, basi. Lakini siku moja akiwa kazini, Anita aliupata ujumbe wa maandishi kwenye simu yake ya mkononi, kutoka kwa mwendesha bodaboda, Don, aliyekuwa anampa habari za mwenendo wa John Bosho na Getruda.


Ni ujumbe ambao uliozidi kumtia jereha moyoni mwake, hasa ukizingatia alikuwa ameshaanza kusahau! Ujumbe ule ulisomeka kwenye kioo cha simu, “Tafadhali dadangu, Anita…nenda Max Bar, Ilala, utawakuta John na Getruda, usifanye fujo. Ninachotaka ni uhakikishe kuwa mchumbako anakusaliti…”


Baada ya kuusoma ujumbe ule, Anita alichanganyikiwa sana, na hamu ya kufanya kazi ikamwisha. Akaamua kuaga kazini, akidai alikuwa amepigiwa simu ya dharura kutoka nyumbani. Akauchukua mkoba wake na kuupachika kwapani na kushuka kwa lifti hadi alipofika chini kabisa katika ghorofa ya mwisho. Akaelekea katika maegesho ya teksi yaliyoko upande wa pili wa Barabara ya Lumumba. Akakodi teksi hiyo impeleke Ilala, wakati huo ikiwa ni saa tisa za alasiri.


Anita alikuwa ameamua jambo moja tu, kuwafuata na kuwavamia ili wajue kwamba alikuwa ameshawashtukia, na pia auvunje uhusiano wa uchumba mara moja, ikiwa ni pamoja na kuivua ile pete ya uchumba na kumrudishia John Bosho. Kutokana na usumbufu wa foleni ya magari barabarani, hatimaye wakafika Ilala, kando ya Barabara ya Uhuru, na pale Anita akashuka na kumlipa dereva nauli yake, na yeye akachanganya miguu kuelekea usawa wa mlango wa kuingilia ndani ya Max Baa.


Mapigo ya moyo wake yaliongezeka na mwili kumtetemeka kwa hasira, lakini kila mtu aliyekutana naye, hakuna aliyemshtukia kama alikuwa katika hali kama ile. Alasiri hiyo wateja walikuwa ni wengi ndani ya baa ile maarufu, ambayo hutumiwa na wafanyabiashara wengi wanaoingia kuburudika baada ya shughuli za kikazi za kila siku.


Baada ya kuingia ndani, Anita aliyatupa macho pande zote za mle ndani ya baa, na kwa bahati nzuri alimwona Getruda na John wamekaa kwenye kona iliyokuwa upande wa kushoto, karibu kabisa na kaunta ya kuuzia vinywaji. Hasira zikaongezeka, hivyo akaanza kuvuta hatua moja baada ya nyingine kuwafuatilia pale walipokuwa wamekaa!


Ni kuanzisha tibwili!


      ********


JOHN Bosho na Getruda walikuwa wamezama katika mazungumzo yao, huku Getruda akiwa amempa mgongo, na John Bosho amekaa upande wa nyuma akiangalia watu wanapoingia. Meza yao ilikuwa na chupa kadhaa za bia, ambao walikuwa wanakunywa.


Kwa muda ule nishai ya pombe ilikuwa imeshaanza kuwaingia wote hasa ukizingatia walikuwa wameanza kunywa muda mrefu, tokea saa nane za mchana,  ikiwa ni yeye John aliyemwita Getruda baada ya kumpigia simu na kumsisitiza wakutane hapo! Ama kweli alikuwa ameshanogewa naye!


John Bosho alikuwa wa kwanza kumwona Getruda alivyokuwa anaingia. Akashtuka na kujiuliza imekuwaje awe pale kwa muda ule? Hata hivyo  akabaki akimwangalia jinsi Anita alivyokuwa anawajongelea. Getruda naye alishangaa baada ya kumwona John amepigwa na bumbuwazi huku akiangalia nyuma yake! Ndipo naye akageuka kuangalia nyuma!


Akamwona Anita!                                                                   


Akashtuka sana!


 Abaki ameachama mdomo wake!


Anita akavuta kiti  na kukaa huku akipumua kwa nguvu!


“Habari zenu…” Anita akawaambia huku akiwa bado amesimama karibu yao.

0 Comments

banner

Ahsante kwa kutembelea zotekali blog ili kuwa karibu nasi kila wakati Jiunge katika kurasa zetu zamitandao ya kijamii  facebook , Twitter, Instagram na Youtube  NI BUREE