Simulizi : muuaji asakwe...... sehemu ya pili

 Mtunzi ni: Patrick J. Massawe



Utangulizi


Mwanamke mrembo anauawa ndani ya bafu, nyumbani kwake, eneo la Tabata, Jijini Dar es Salaam. Kwanza kabisa, muuaji huyo katili alimtumia ujumbe wa vitisho muda mfupi tu kabla ya kutekeleza mauaji hayo. Pia, muuaji huyo alimbaka mrembo huyo kabla ya kumuua. Upelelezi wa Jeshi la Polisi, unafanyika mara moja. Msako mkali dhidi ya muuaji huyo unafanyika, na inagundulika siri nzito iliyojificha nyuma ya mapazia kuhusiana na kifo hicho chenye utata. Kama kawaida, mtunzi wako mahiri,  PATRICK J. MASSAWE anatiririka na hadithi hii ya kusisimua.     Fuatilia mpaka mwisho wake…


“Ndiyo, nitahama kumfuata mume.”


“Je, ukichumbiwa na kupangiwa chumba, utakubali?”


“Inategemea…” Anita akasema na kuongeza. “Mchumba akiwa mwaminifu nitakubali, maana siku hizi wanaume wengi siyo waaminifu kabisa…”


“Una maana gani kusema hivyo?”


“Nina maana kuwa, ninaweza kuchumbiwa na mchumba ambaye tutakuwa tumekubaliana. Halafu ananipangia chumba, kumbe mchumba mwenyewe anaweza kuja kuwa mwongo tu wa kunipotezea muda wangu, na baadaye kunitelekeza baada ya kunitumia vya kutosha!”Anita akamwambia John.


“Unalosema ni kweli,” John Bosho akasema na kuongeza. “Lakini siyo wanaume wote wanaofanya hivyo.”


“Na mimi sikusema wote, John…” Anita akamwambia baada ya kujua John alikuwa ana maana gani!


Alikuwa anajipigia debe yeye mwenyewe!


“Ok, tuyaache hayo. Je, unaweza kuwa na nafasi siku gani, ili tuweze kuongea mambo mengi na kufahamiana zaidi?” John Bosho akamuuliza Anita.


“Siku ambayo nina nafasi, ni Jumapili…” Anita akamwambia.


“Basi, nakuomba sana tukutane Jumapili inayokuja…”


“Tukutane wapi?”


“Naomba tukutane Zungwa Beach Hotel, Oysterbay. Hii ni sehemu iliyotulia sana, hakuna vurugu kama hoteli nyingine za uswahilini.”


“Sawa, kama umechagua twende huko, mimi sina kipingamizi.”


“Na kuhusu usafiri, nitakupitia sehemu, mbali kidogo na nyumbani kwenu, halafu tuongozane wote.”


“Hakuna shaka, na mengine tutawasiliana kwa simu…”


John Bosho na Anita walikaa hapo New Africa Hotel, huku wakiendelea kula na kunywa vinywaji baridi. Hapo waliongea mengi, hadi walipomaliza kula, ndipo walipotoka tayari kurudi katika sehemu zao za kazi, hivyo wakatoka nje tayari kwa kuondoka.


Hakika John Bosho alikuwa ameridhika sana baada ya kukutana na kimwana yule aliyekuwa amemwingia rohoni mwake. Na zaidi ni ile kumkubalia kukutana naye siku ya Jumapili kule Zungwa Beach Hotel, ili aweze kumjulisha azma yake. Baada ya kupanda gari, wakaondoka kumrudisha Anita kazini kwake, na yeye akaendelea na shughuli zake. Alishaamua kufanya urafiki na Anita, na hata ikiwezekana awe mke wake hapo baadaye.


        *******


SIKU ya Jumapili ilifika, na kama walivyokuwa wameahidiana, John Bosho na Anita walikwenda Zungwa Beach Hotel, iliyoko ufukweni mwa Bahari ya Hindi, kutembea na kupumzika katika kuifurahia mwisho wa wiki. Kama kawaida, John Bosho alimpitia nyumbani kwao, Kiwalani na kumchukua kwa gari lake.


Siku hiyo Anita alikuwa ameupara vizuri na kuonekana ule uzuri wake waziwazi kitu ambacho kilimvutia sana John.Baada ya kufika kwenye hoteli hiyo ya kifahari, iliyoko ufukweni mwa Bahari ya Hindi, siyo mbali sana na ufukwe wa Coco, John alilipaki gari katika sehemu ya maegesho ambapo palikuwa na magari mengine.


Baada ya kulipaki, wote wakashuka na kuelekea sehemu ya nyuma ya hoteli kwa mwendo wa taratibu kama vile wapenzi wawili wanaopendana, ambapo palikuwa na sehemu nzuri ya kupumzikia, iliyokuwa na mandhari nzuri hasa ukizingatia ilikuwa karibu kabisa na bahari.


Sehemu hiyo waliyokuwa wamekaa John Bosho na Anita, palikuwa na viti vilivyokuwa ndani ya kibanda cha makuti, waliagiza chakula na vinywaji, ambapo waliendelea kula na kunywa taratibu. Hapo ndipo John Bosho alipoanza kumwaga sera zake kwa Anita, katika kumwingiza katika mstari ulionyooka.


Vilevile walikuwa wakiongea mambo mengi na kujikuta wakiingia katika dimbwi la mapenzi, kwani kutokana na jinsi John Bosho alivyokuwa akipangilia maneno yake, na Anita alijikuta akikubali kila alichoambiwa. Walipomaliza kula na kunywa, walipanga chumba cha muda ndani ya hoteli hiyo ya kifahari, ambapo walipumzika humo na kujiliwaza kimapenzi kwa zaidi ya saa mbili.


Walipomaliza starehe yao ya kiutu uzima, walioga na kuvalia tena nguo zao, halafu wakaondoka kurudi katikati ya jiji. Walisumbuliwa sana na foleni ya magari barabarani, lakini John alimrudisha Anita nyumbani kwao, Kiwalani, akiwa salama. Hakika, kwa upande wa John, alikuwa amefurahi sana baada ya kumnasa mwanadada huyo mrembo, ambaye alifanana na mazingira yake anayoishi, akiwa ni mtu mwenye fedha za kutakata.


Kuanzaia hapo, John Bosho aliapa kuwa hatokubali ampoteze Anita, na atammiliki awe wake daima, na hakuna mwanaume mwingine atakayemwingilia katika penzi lake change!


        ********


BAADA ya miezi mitatu hivi, John Bosho na Anita walishakuwa marafiki na kushirikiana katika mapenzi. Wakajikuta kila mmoja akimhitaji mwenzake, kwa kila anapopata nafasi.


Hata hivyo ile kero ya kukutana katika mahoteli makubwa au katika n yumba za kupanga, kama vile Lojingi, hazikuwafurahisha wote wawili, hivyo John akaamua kumpangia Anita nyumba ya maana itakayomfaa, ambapo hakutaka apate shida.


Anita alifanikiwa kupata nyumba ya kupanga eneo la Tabata Mawenzi, ambapo akiwa mpenzi wake, John Bosho, akiwa ni mtu anayefahamika sana, alitumia madalali maarufu, ambao walimtafutia nyumba hiyo iliyokuwa katika kiwango alichokipenda.


Ni nyumba ndogo iliyojengwa kifamilia, ikiwa na vyumba viwili, sebule na stoo. Pia, huduma za choo zilikuwa mlemle ndani. Akalipa kodi ya mwaka mzima, na Anita akahamia mara moja, kutoka Kiwalani, nyumbani kwa wazazi wake alipokuwa anaishi kwa muda mrefu.


Mbali ya kumpangia nyumba hiyo, pia alimnunulia samani zote za ndani. Ni samani alizozinunua katika duka moja linalouza samani za gharama, lililopo  katika Barabara ya Nyerere. Baada ya kumfanyia yote yale, sasa John akapumua na kufurahia kummiliki mwanadada yule mrembo aliyekuwa anamezewa mate na wanaume wengi!


Kwa vile nyumba hiyo ilikuwa na usalama wa hali ya juu, John Bosho alikuwa anakwenda mara kwa mara na kupumzika, huku pia akijaribu kujikwepesha asijulikane na watu wengi sana ukiwa ndiyo utaratibu wake aliokuwa amejiwekea. Kufahamiana na watu ovyo, wataijua siri yake!


Ni mtu wa aina gani!


        ********


MARA baada ya John na Anita kuunganisha mahisiano na uchumba, Anita aliona ni vyema akutane na mama yake mzazi ili amfahamishe kuhusu jambo hilo ambalo kwa upande wake aliona kuwa ni la kheri kwani ni wanaume wachache sana siku hizi wanaopenda kuoa, na pia ni wanawake wengi ambao hawaolewi, hivyo ni bahati yake ya pekee ambayo kamwe hakupenda kuikosa.


Hivyo basi, Anita alimwomba mama yake wakutane faragha ili aweze kumdodosea. Siku hiyo ya Jumapili walikutana ndani ya sebule nadhifu, nyumbani kwao Kiwalani, ambapo Anita alimtembelea mama yake huyo, Bi. Matilda, ukiwa ni utaratibu wake wa kawaida aliokuwa amejiwekea.


Baada ya kufika pale nyumbani, aliwakuta wazazi wake, baba na mama yake ambao aliwasalimia, wakaongea mengi tu. Anita alihudumiwa kinywaji baridi huku akiendelea kunywa taratibu, na ndipo alipoanza kumweleza mama yake juu ya azma yake ile.


“Mama, nimekuomba kukutana na wewe, kwani nina maongezi muhimu sana,” Anita alimwambia mama yake ambaye walikuwa wamekaa naye kwenye sofa kubwa hapo sebuleni.


“Maongezi gani mwanangu,” mama yake, Bi. Matilda akamuuliza.


“Napenda kukujulisha kuwa nimepata mchumba,” Anita akamwambia huku akiunda tabasamu pana.


“Oh, umepata mchumba mwanagu?” Bi. Matilda, mama yake akamuuliza huku naye akiunda tabasamu pana.


“Ndiyo, mama, si unajua umri unazidi kwenda?”


“Ni kweli mwanangu, umri unazidi kwenda. Ni vizuri sana kama utaolewa mapema na kupata watoto mapema, kwani ukichelewa zaidi ya miaka mitatu kutokea sasa, basi ujue umezeeka! Itabidi uolewe na mtu wa makamo ambaye siyo kijana tena!”


“Na ndiyo hilo sitaki mama…”


“Basi, hilo ni jambo la heri,” mama yake akasema na kuongeza. “Lakini cha muhimu ni vyema kama unamuamini huyo mchumba, basi, afanye taratibu zote za kuja kujitambulisha kwetu na mambo mengine yafuata.”


“Yeye pia ana hamu kubwa sana ua kuja kujitambulisha,” Anita akasema na kuongeza. “Ukweli ni kwamba ni mtu ninayemuamini, na siamini kama atakuwa ni mwanaume mwongo.”


“Vizuri, nashukuru kwa kunieleza hayo. Mimi nitakaa na baba yako, halafu nimweleze jambo hili,” mama yake akamwambia kwa kumpa matumaini.


“Sawa, mama, nitashukuru sana.” Anita akasema.


Baada ya kumaliza mazungumzo yao ambayo hayakuichukua muda mrefu, Anita alibaki akimalizia kinywaji chake na pengine kuongelea mambo mengine yanayohusu maisha kwa ujumla.


********


WALIONEKANA ni wapenzi wawili waliopendana sana. Kila sehemu, John na Anita walikuwa wakifuatana wote, iwe kwenye starehe au hata kufanya manunuzi katika maduka mbalimbali ya bidhaa za chakula na hata nguo na vipodozi, jijini Dar es Salaam.


Baada ya mapenzi yao kukolea haswa, ndipo John Bosho alipofanya utaratibu mzima wa kujitambulisha kwa wazazi wa Anita. Alitafuta wazee wanaofahamika, akajitambulisha, utambulisho ambao ulifuatiwa na sherehe ndogo iliyofanyika katika ukumbi mmoja maarufu ulioko eneo la Kiwalani.


Hivyo basi, kuanzia hapo John Bosho akawa anafahamika kama mchumba, na mume mtarajiwa wa Anita, mwanadada mrembo, aliyekuwa ana husudiwa na wanaume wengi, ambao nao walipenda wammiliki.  Na ili kuondoa udhia kabisa, akaamua kumvisha pete ya uchumba ya gharama kubwa, iliyotenezwa kwa dhahabu, ili ijulikane kuwa ni mchumba wake halali, asije akaporwa na wanaume wengine wenye uchu mkali.


Mbali ya wazazi wake kumfahamu John, pia ndugu na jamaa nao walimjua kuwa alikuwa katika mpango wa kuja kumuoa Anita. Ikawa ni faraja kubwa kwa Anita kupata mchumba, heshima ikawa kwake, kwani aliheshimiwa na watu wote, wanaume kwa wanawake, kwa kujua sasa alikuwa amekata shauri la kuolewa na kuondokana na maisha yap eke yake.


Hali ilendelea kuwa hivyo, na hata ofisini kwake alipokuwa anafanya kazi, wafanyakazi wenzake walikuwa wameshajua kuhusu mwenzao kupata mchumba, kiasi kwamba hata wale mabosi waliokuwa na kijicho pembe cha matamanio, waliacha kabisa tabia hiyo ya kumtaka kimapenzi!


Mapenzi ya John Bosho na Anita yalikolea kadri siku zilivyokuwa zinakwenda. Muda wote huo, Anita alikuwa anajua kuwa mchumba wake huyo alikuwa ni mfanyabiashara mkubwa mwenye biashara nyingi, lakini upande wake wa pili hakuujua undani wake kwa vile alikuwa ni mtu anayefanya shughuli zake hizo kwa siri sana.


********      


SIKU za nyuma, Anita na mwanadada, Getruda walikuwa ni marafiki wakubwa, waliokuwa wamesoma wote katika Shule ya Sekondari ya Tambaza, jijini Dar es Salaam. Lakini baada ya kumaliza masomo yao ya sekondari, kila mmoja aliendelea na shughuli zake, ambapo Anita alijiunga na Chuo cha Uhasibu, Chang’ombe, na Getruda akajiunga na kampuni moja ya simu za mkononi, akiwa Afisa Masoko.


Hata hivyo urafiki wao ulikuwa haujafa, kwani walikuwa wakitembeleana mara kwa mara wanapopata nafasi. Walionekana kama vile walikuwa ni ndugu waliozaliwa tumbo moja, mambo yalikuwa hayohayo mpaka wakati mwingine walipojikuta wakiwa bize sana na shughuli zao, kiasi cha kutoweza tena kuonana mara kwa mara zaidi ya kuwasiliana kwa simu zao za mkononi.


Siku moja ya Jumamosi, John Bosho, Anita na Getruda, walijikuta wamekutana katika viwanja vya starehe, wakijirusha na pengine kusuuza makoo yao kwa vinywaji. Walikutana kwenye Ukumbi wa Amana Club, Ilala, ambapo John Bosho alikuwa amekwenda na Anita kwa ajili ya kuburudika na Muziki wa Dansi wa Msondo Ngoma, unaoporomoshwa na Bendi ya Muziki wa Dansi ya Msondo.


John Bosho alikuwa ni mpenzi wa ‘Msondo,’ ambapo hakupenda kukosa hata mara moja katika siku za mwisho wa wiki. Wakiwa wamekaa katika meza yao, Anita aliweza kumwona Getruda akicheza muziki akiwa peke yake. Akanyanyuka baada ya kumuaga John na kumwendea Getruda pale alipokuwa na kumshika begani.


“Getu…” Anita akamwita kwa sauti ndogo huku akimgusa.


“Oh, Anita…waooo!” Getruda akasema huku akinyanyuka na kumkumbatia Anita, na pia akishangaa kumuona katika eneo lile.


“Za siku?”


“Nzuri, sijui wewe?”


“Mimi safi…”


“Uko na nani?” Getruda akamuuliza Anita.


“Niko na mchumba wangu, twende ukamfahamu…” Anita akamwambia huku akitabasamu!


Wote wawili wakaongozana huku wameshikana mikono yao, hadi pale kwenye kiti alipokaa John Bosho. Wakasalimiana na kutambulishana.


“Getu, huyu ni mchumba wangu, anaitwa John…” Anita akamtambulisha kwa mchumba wake.


“Nashukuru sana kumfahamu…” Getruda akasema huku akimwangaliam John ambaye naye alikuwa anamwangalia kwa jicho la kisanii!


“John, huyu ni rafiki yangu, anaitwa Getruda, ambaye tumesoma naye shule ya Sekondari…” Anita akamwambia John, ambaye bado alikuwa akimwangalia Getruda!


“Nashukuru kumfahamu…” John Bosho akamwambia na kuendelea. “Anaishi wapi hapa jijini Dar es Salaam?”


“Anaishi Ilala, mtaa wa Moshi…siyo mbali sana kutoka hapa Amana…” Anita akasema.


“Oh, nashukuru sana,” John akasema huku akimpa mkono Getruda. Halafu akaendelea kusema. “Mimi ndiye John Bosho, kama ulivyotambulishwam, ninaishi huko Ukonga, lakini mwenzangu anaishi Tabata Mawenzi.”


“Nashukuru kwa kufahamiana…” Getruda akasema huku bado akiwa ameunda tabasamu pana.


Getruda alikuwa ni mwanamke aliyeumbika. Ni mwanamke mwenye lile umbile tata linalowasumbua wanaume wengi sana, akiwa amejaza makalio yaliyofuatiwa na nyonga iliyotanuka na umbile la namba nane! Kila akitembea makalio yalikuwa yanatikisika pasipo mwenyewe kupenda!


Hakika umbile hilo la Getruda, lilimsumbua sana John Bosho. Basi, tokea muda huo, akili yake ilikuwa haifanyi kazi tena baada ya kumwona Getruda akiwa na  lile gauni laini na la kubana alilovaa, ambalo liliruhusu mzigo wote wa makalio umwagike nyuma!


Huo ulikuwa mtego!


Siyo kwamba Anita alikuwa mwanamke mbaya ksura, kimaumbile au hata tabia, hasha. Isipokuwa ile ilikuwa ni tamaa ya wanaume wengi wasiokuwa na ustahimilivu baada ya kuona vitu kama vile! Lakini ukweli unabaki kwamba Getruda kwa usiku ule alikuwa tishio, na alimtamanisha kila mwanamke yeyote rijali!


Usiku huo waliburudika kwa muda mrefu huku wakiongea hili na lile. Kwa wakati wote John Bosho alikuwa akicheza muziki na wanawake wote wawili, Anita na Getruda; wala Anita hakuwa na wivu wala kumtilia mashaka mchumba wake, kwamba anaweza kumtaka kimapenzi rafiki yake huyo, kumbe huku nyuma, John alikuwa ameshamhusudu Getruda, hivyo akaamua kuwa ni lazima ampate!


Kazi hiyo!


Ndipo John Bosho alipopata wasaa wa kumuulizia sehemu anayoishi, nyumba na mtaa. Bila kutambua nia yake, Getruda alimjulisha kuwa yeye anaishi mtaa wa Moshi, Ilala, nyumba namba 003. Mbali ya kumfahamisha sehemu hiyo anayoishi, pia walipeana namba za simu zao za mkononi, ambapo wangeweza kuwasiliana kwa kusalimiana na kutakiana heri kwa ujumla.


Ukweli ni kwamba, Getruda hakujua kwamba John Bosho alikuwa ana nia mbaya dhidi yake, kwani alikuwa amechukua namba zake za simu ya mkononi, akiwa na lengo lake. Hivyo baada ya burudani ya muziki wa danisi kumalizika, ndipo wote walipoondoka kwa gari lao, ambapo John alimpitisha Getruda nyumbani kwake, mtaa wa Moshi, na kumwacha.


Akiwa ni mwenyeji tosha ndani ya jiji la Dar es Salaam, John Bosho aliweza kuitambua ile nyumba aliyokuwa amepenga Getruda, akaitia alama kichwani mwake. Baada ya kumshusha Getruda, wenyewe wakarudi  Tabata Mawenzi, alikompangia nyumba Anita, tayari kwa kupumzika. Siku hiyo John Bosho alilala hukohuko nyumbani kwa Anita.


********      


AKILI ya John Bosho hakutulia. Ilikuwa bado imezama kimapenzi kwa kimwana Getruda, rafiki yake mkubwa Anita, mchumba wake. Tamaa na uchu ulikuwa umemtawala pasipo kuweka tahadhari yoyote, hasa akilifikiria lile umbile tata alilokuwa nalo Getruda, ambalo likuwa limefichwa ndani ya magauni makubwa kama dera au nguo za kubana, kwa vyovyote alidhamiria kulionja.


Akiwa ni mtu mwenye kujiamini, na mwenye fedha vilevile, John Bosho hakukaa kimya, kwani aliamua kumtafuta Getruda, rafiki yake Anita, ili amweleze azma yake ile ya kumtaka kimapenzi, hata kwa kutumia fedha. Wakati huo hakuona ubaya wowote kumtaka, kwani yeye aliamini kuwa ana haki ya kumtaka kila mwanake anapopenda! Hakuna kinachoshindikana mbele ya fedha!


Kwa vile John Bosho alikuwa na namba za simu ya mkononi ya Getruda, basi akampigia na kumwomba wakutane sehemu watakayopanga, kwani alikuwa na mazungumzo naye, akiwa kama shemeji yake. Kwa vile Getruda hakumtilia mashaka, basi walikubaliana kukutana pale Msewa Bar & Lodging, iliyoko Buguruni, kunako majira ya saa moja za jioni. Hata hivyo, Getruda alikuwa akijiuliza kuwa John Bosho alikuwa anamwitia nini mpaka wakutane katika sehemu hiyo? Lakini akavuta subira mpaka watakapokutana.


Getruda alipotoka kazini jioni, aliamua kupitia nyumbani kwake, mtaa wa Moshi, Ilala, kwanza, halafu akaoga na kuvalia nguo nyingine nadhifu ukizingatia sehemu yenyewe aliyokuwa anakwenda, ilikuwa na mkusanyiko wa watu wengi. Baada ya kumaliza kuvalia, Getruda akatoka na kutembea kwa miguu hadi alipofika katika barabara kuu ya Uhuru, inayotokea katikati ya jiji kuelekea maeneo ya Buguruni na kwingineko.


Sehemu hiyo kulikuwa na teksi kadhaa zilizokuwa zimepaki zikisubiri wateja, hivyo Getruda akakodi teksi moja wapo na kumwambia dereva ampeleke Buguruni. Dereva akaiondoa teksi na kuifuata barabara ile ya Uhuru hadi alipofika Buguruni, eneo la Sokoni, halafu akamshusha Getruda. Sehemu hiyo palipokuwa na pilikapilika za watu wengi, hivyo nusu iliyobaki ambayo si mbali sana na ilipo Msewa Bar & Lodiging, alitembea kwa miguu kwa mwendo wa taratibu hadi alipoingia ndani ya baa ile maarufu.


Alipoingia tu, akaangaza macho yake pande zote, lakini hakumwona John Bosho kama walivyoahidiana kukutana katika eneo lile la baa. Hata hivyo akachukua simu yake na kumpigia, ili kujua alipo kwa wakati ule, na John akamjulisha sehemu ile alipokuwa na kumwambia amfuate ndani ya chumba maalum kilichokuwa na huduma zote zinazohitajika.


 Ni chumba kilichokuwa upande wa nyuma ya baa ile, ambapo palikuwa na vyumba vingine kwa ajili ya starehe za muda mfupi au kulala mpaka asubuhi, hivyo Getruda akaelekezwa na wahudumu, na kupelekwa hadi kule nyuma ya baa, ambapo aliingia ndani ya chumba kile na kumkuta John Bosho amekaa kwenye sofa dogo, mbele yake kukiwa na meza ndogo iliyokuwa na vinywaji.


Kilikuwa ni chumba kikubwa, kilichokuwa na seti moja ya makochi, friji ndogo, runinga, choo na bafu vilikuwa mlemle. Pia, palikuwa na sebule iliyokatwa kwa pazia kubwa lililotenga chumba kile, ambapo ndani kulikuwa na kitanda kikubwa cha futi sita kwa sita.


“Karibu Getruda,” John Bosho akamwambia huku akitabasamu.


“Ahsante…” Getruda akasema huku bado amesimama!


 Alikuwa akishangaa kumkuta shemeji yake huyo, John Bosho akiwa katika sehemu kama ile yap eke yake!


Chumbani!


“Mbona unasita?” John Bosho akamuuliza huku akinyanyuka kutoka pale kwenye sofa alipokaa.


“Lazima nishangae…” Getruda akamwambia.


“Unashangaa nini sasa?”                                            


“Mbona hapa ni chumbani?”


“Ndiyo, ni chumbani….” John Bosho akamwambia na kuendelea. “Ndivyo nilivyoamua, si unajua kuwa hapa kuna utulivu, tofauti na kule kwenye baa?”


“Yaani umeniita kwa mazungumzo ya kuongelea chumbani?” Getruda akamuuliza. “Wala usihofu shem…” John akamwambia huku akimkalisha

0 Comments

banner

Ahsante kwa kutembelea zotekali blog ili kuwa karibu nasi kila wakati Jiunge katika kurasa zetu zamitandao ya kijamii  facebook , Twitter, Instagram na Youtube  NI BUREE