Chadema yamng’ang’ania Spika Tulia kesi ya akina Mdee

 CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema), kimesema kinawasiliana na mawakili wake ili kuangalia namna ya kufanyia kazi hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu, Masjala Kuu ya jijini Dar es Salaam, dhidi ya kesi iliyofunguliwa na waliokuwa wanachama wake 19, wakiongozwa na Halima Mdee. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).



Kauli hiyo imetolewa jana Alhamisi na Mkurugenzi wa Mawasiliano, Itifaki na Mambo ya Nje Chadema, John Mrema, muda mfupi baada ya hukumu hiyo kutolewa mahakamani hapo mbele ya Jaji Cyprian Mkeha, katika kesi ya madai Na. 36/2021, iliyofunguliwa na Mdee na wenzake kupinga uamuzi wa  kuvuliwa uanachama wa Chadema.


“Tumepokea hukumu iliyotolewa leo (jana), kwamba uamuzi wa kuwafukuza uanachama waliokuwa wanachama wetu 19 uliofanywa na Kamati Kuu ya chama umeendelea kusimama na mahakama imekubaliana kuwa taratibu zote za katiba ya Chadema na sheria za nchi zilifuatwa kikamilifu na kamati katika kuchukua uamuzi huo,” imesema taarifa ya Mrema.


Taarifa hiyo imesema “kwamba, maamuzi ya Baraza Kuu kuhusu rufaa yamefutwa na hivyo linapswa kukaa upya kusikiliza rufaa. Lakini kamati kuu ilishawafukuza uanachama na uamuzi wa jaji kasema wazi upo sahihi.”


Kufuatia hukumu hiyo, Chadema imemkumbusha Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, kufanyia kazi hukumu hiyo kwa kuwatoa bungeni wabunge hao viti maalum, ikidai kuwa hawana chama.


“Hivyo basi, kwa hatua ya sasa chama kinawasiliana na mawakili wake ili kutafakari hatua za kuchukua ikiwa ni pamoja na kumkumbusha Spika wa Bunge kuhusu utekelezaji wa uamuzi wa kamati kuu ya chama wa tarehe 27 Novemba 2020, kwani mahakama imethibitisha kuwa walishafukuzwa uanachama kihalali na taratibu zote zilifuatwa,” imesema taarifa hiyo.


Chadema kimetoa wito huo dhidi ya Spika Tulia, baada ya kiongozi huyo wa Bunge kusema wabunge hao wataendelea kubaki bungeni hadi mahakama itakapotoa uamuzi dhidi ya kesi waliyofungua mahakamani.


Kwenye kesi hiyo, Mdee na wenzake ambao wote ni wabunge viti maalum, walikuwa wanapinga uamuzi wa Kamati Kuu ya Chadema kuwavua uanachama kwa kosa la usaliti, kwa madai kuwa hawakupewa nafasi ya kusikilizwa.


Lakini pia walikuwa wanapinga uamuzi wa Baraza Kuu la Chadema, kutupitilia mbali rufaa walizokata kupinga uamuzi wa kamati hiyo kuwatimulia mbali.


Katika hukumu hiyo, mahakama ilitoa uamuzi wa kwamba, maamuzi ya kamati kuu ya Chadema kuwafukuza Mdee na wenzake, yalikuwa halali.


Isipokuwa uamuzi wa rufaa zao kutupiliwa mbali ulikuwa batili,  kwa kuwa kulikuwa na upendeleo kutokana na baadhi ya wajumbe walioshiriki kikao cha kamati kuu cha kuwafukuza, walishiriki pia katika mkutano wa baraza kuu.


Wakati wa mwenendo wa kesi hiyo katika nyakati mbalimbali, Mdee na wenzake walionesha kutoridhishwa na baadhi ya vigogo wa Chadema kushiriki katika kikao kilichowafukuza na kile kilichokuwa kinafanyia kazi rufaa yao, wakidai uwepo wao ulishinikiza wajumbe wa Baraza Kuu la chama hicho kukazia uamuzi wa awali wa kuwafukuza uanachama.


Miongoni mwa vigogo wa Chadema ambao Mdee na wenzake walikuwa wanawalalamikia walishiriki baraza hilo,  ni Katibu Mkuu wa chama hicho, John Mnyika na Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Freeman Mbowe.

0 Comments

banner

Ahsante kwa kutembelea zotekali blog ili kuwa karibu nasi kila wakati Jiunge katika kurasa zetu zamitandao ya kijamii  facebook , Twitter, Instagram na Youtube  NI BUREE